Aina za vitenzi katika Kiswahili

Vitenzi ni nini?

Vitenzi ni aina ya neno linaloeleza kitendo au hali inayofanywa na mtendaji.

Aina za vitenzi

  • Vitenzi halisi
  • Vitenzi vikuu
  • Vitenzi visaidizi
  • Vitenzi vishirikishi
  • Vitenzi sambamba

Vitenzi halisi

Vitenzi hivi huwa na maana kamili katika sentensi, na hutumika peke yao katika sentensii bila kuandamana na vitenzi vingine.

Huwa na viambishi kabla na baada ya mzizi.

Mfano

Yeye anasoma. – ‘anasoma’ ni kitenzi halisi na kina kiambishi; a-kiambishi cha nafsi, na- wakati, som- mzizi, a- kiishio.

Kesho tutalima. – tu-kiambishi cha nafsi, ta- wakati, lim- mzizi, a- kiishio

Tunakimbia kwenda shule. n.k.

Vitenzi vikuu

Vitenzi vikuu hubeba maana kamili ya sentensi. Kitenzi kikuu lazima pawe na vitenzi kadhaa kwa sentensi ndipo kiwepo.

Mfano

Kifaru alikuwa akicheza ngoma asubuhi. – ‘alikuwa ‘ imetumika kama kitenzi kisaidizi. Kitenzi kikuu ni ‘akicheza’.

Sisi tulikuwa tunalima. – Tunalima ni kitenzi kikuu kwa sababu kinabeba maana kuu ya sentensi na pia kimeandamana na kitenzi kisaidizi ambacho ni “tulikuwa”

Aliponipigia, nilikuwa ninatazama filamu. – ‘ninatazama’ ni kitenzi kikuu, kimebeba maana kamili ya sentensi. ‘nilikuwa’ ni kitenzi kisaidizi.

Anapenda kutazama runinga. – ‘kutazama’ ni kitenzi kikuu, kimebeba maana kamili ya sentensi. ‘anapenda’ ni kitenzi kisaidizi.

Yazingatie yale niliyokwambia ili usije ukayasahau. – ‘ukayasahau’ ni kitenzi kikuu, kimebeba maana kamili ya sentensi. ‘usije’ ni kitenzi kisaidizi.

Vitenzi visaidizi

Huja kabla ya vitenzi vikuu au vitenzi halisi. Vitenzi visaidizi vinatoa msaada kwa vitenzi vikuu ili kuleta maana inayokusudiwa.

Hivi ni kama: kuwa, kuweza, kwenda, kupasa, kuwahi, kuja, kupenda, kwisha, kupata n.k.

Mifano wa sentensi

Sisi tulikuwa tunalima – Tulikuwa ni kitenzi kisaidizi: Kimekuja kabla ya kitenzi kikuu “tunalima” na pia kinasaidia katika kubeba maana ya sentensi.

Aliponipigia, nilikuwa ninatazama filamu. – kitenzi ‘nilikuwa’ husaidia kitenzi kikuu ‘ninatazama’.

Anapenda kutazama runinga. – kitenzi ‘anapenda’ kinakuja kabla na kinasaidia kitenzi kikuu ‘anatazama.

Yazingatie yale niliyokwambia ili usije ukayasahau.

Kifaru alikuwa akicheza ngoma asubuhi. – ‘alikuwa ‘ imetumika kama kitenzi kisaidizi. Kitenzi kikuu ni ‘akicheza’.

Vitenzi vishirikishi

Vinaitwa vitenzi vishirikishi kwa sababu hushirikisha kitu au mtu na hali au tabia fulani.

Vitenzi viki vimegawika katika aina mbili:

(a) vitenzi vishirikishi vikamilifu

(b) vitenzi vishirikishi vipungufu

Vitenzi vishirikishi vikamilifu

Huchukua viambishi vya ngeli, nafsi au vya wakati. Vitenzi hivi vinaweza kujisimamia peke yake au vinaweza kufuatiliwa na vitenzi vikuu.

Mifano

Babu angali na nguvu – ‘angali’ ni kitenzi kishirikishi kikamilifu maana kinashirikisha nomino “Babu” na hali ya “kuwa na nguvu” na pia kina viambishi ‘a-‘.

Chakula ndicho nguzo ya maisha. – ‘ndicho’ ni kitenzi kishirikishii kikamilifu maana kinashirikisha nomino ‘Chakula’.

Jibwa ndilo lilibweka asubuhi. – ‘ndilo’ ni kitenzi kishirikishii kikamilifu maana kinashirikisha nomino ‘Jibwa’.

Kanisani ndiko kuna sherehe yake. – ‘ndiko’ ni kitenzi kishirikishii kikamilifu maana kinashirikisha nomino ‘Kanisa’.

Vitenzi vishirikishi vipungufu

Havichukui viambishi

Huwa ni silabi moja tu mfano; zi, ki, li, vi, ni, si n.k

Mfano

Kalamu i mezani pako.

Nguo nzuri zi sandukuni.

Baba yangu ni Daktari.

Babu yu chumbani.

Zena ni mwerevu.

Jugo si mchezaji.

Vitenzi sambamba

Vitenzi sambamba hutokea katika mfululizo wa vitenzi visaidizi na vikuu.

Mfano

Yohana angekuwa akisoma angefaulu. – Hapa, ‘angekuwa akisoma angefaulu’ ni vitenzi sambamba.

Wawire alikuwa akiandika insha. – Vitenzi sambamba ni: ‘alikuwa akiandika’, ‘alikuwa’ ni kitenzi kisaidizi na ‘akiandika’ ni kitenzi kikuu.

Mwalimu anafundisha akiandika. – ‘anafundisha akiandika’ ni vitenzi sambamba.

Jemale alikuwa anazungumza akila ofisini. – ‘alikuwa anazungumza akila’ ni vitenzi sambamba.

Ogutu angali anachora vizuri. – ‘angali anachora’ ni vitenzi sambamba, ‘angali’ ni kitenzi kishirikishi kikamilifu na ‘anachora’ ni kitenzi kikuu.  

Related Posts